VPL: SIMBA, YANGA NGOMA DROO 1/10/2016
 
https://rucuso.blogspot.com/2016/10/vpl-simba-yanga-ngoma-droo-1102016.html
Shiza  Ramadhani Kichuya ameifungia Simba bao la kusawazisha katika mechi ya  watani wa jadi iliyomalizika kwa sare ya kufungana goli 1-1 uwanja wa  taifa.
Sare  ya leo inazidi kuipandisha kileleni Simba SC ikifikisha pointi 17,  baada ya kucheza mechi saba, wakati Yanga inatimiza pointi 11 baada ya  kucheza mechi sita.
Katika  mchezo wa leo Yanga walitangulia kwa bao la Mrundi, Amissi Joselyn  Tambwe kabla ya mzalendo, Shizza Ramadhani Kichuya kuisawazishia Simba  SC iliyocheza pungufu kwa muda mrefu baada ya Jonas Mkude kutolewa kwa  kadi nyekundu kipindi cha kwanza.
Goli  hilo lilizua tafrani kwa wachezaji wa Simba kumzonga mwamuzi wa mchezo  huo Martin Saanya hali iliyopelekea kumuonesha kadi nyekundu nahodha wa  Simba Jonas Mkude.
Mashabiki  wa Simba walianzisha vurugu kwa kung’oa viti na kuvirusha uwanjani hali  iliyopelekea polisi kutumia mabomu ya machozi kuleta utulivu ndani ya  uwanja.
Kipindi  cha kwanza kikamalizika Yanga wakiwa mbele kwa goli 1-0 huku Simba  wakiwa pungufu kufuatia Mkude kuoneshwa kadi nyekundu.
Tambwe  alifunga bao lake dakika ya 26, akimalizia pasi ndefu ya beki Mbuyu  Twite na kugeuka mbele ya beki wa Simba, Novat Lufunga kabla ya kufumua  shuti lililomshinda kipa Vincent Angban.
Bao  hilo lilizua kizaazaa, wachezaji wa Simba wakimvaa mwamuzi Martin  Saanya wakidai mfungaji, Tambwe aliushika mpira kabla ya kufunga.
Katika  vurugu hizo, Saanya akamtoa kwa kadi nyekundu Nahodha wa Simba SC,  Jonas Mkude dakika ya 29 kwa sababu ndiye aliyekuwa mstari wa mbele.
Na  mchezo ukasimama kwa takriban dakika tano baada ya mashabiki wa Simba  kuanza kufanya vurugu waking’oa viti na kutupa uwanjani.
Polisi walitumia milipuko kuwatuliza mashabiki hao na mchezo ukaendelea.
Kipindi  cha pili, Simba SC walibadlika pamoja na kucheza kwa nguvu wakafanikiwa  kupata bao la kusawazisha lililofungwa na winga Shizza Kichuya dakika  ya 87 baada ya kona aliyochonga kuingia moja kwa moja nyavuni.



